Social Icons

Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com

bre

Sunday, September 20, 2015

WATU 9 WAJERUHIWA KATIKA VURUGU KATI YA MGOMBEA UBUNGE WA CHADEMA MBEYA MJINI NA WAFUASI WA CCM



Mgombea Ubunge kwa tiketi ya Chadema Jimbo la Mbeya mjini Joseph Mbilinyi akiwa sambamba na dereva wake akibishana na wafuasi wa Chama cha Mapinduzi baada ya kuvamia eneo lao la mkutano wa kampeni za Ubunge katika kata ya Ghana.

Vijana wa boda boda wanaomuunga mkono Joseph Mbilinyi wakizuiliwa na Green Guard wa CCM.

Baadhi ya viongozi wa CCM wakimsihi Joseph Mbilinyi kutoendelea na safari yake na badala yake ageuze lakini bado aliendelea na maamuzi yake.


Wanachama wa CCM waliokuwa kwenye mkutano wa kampeni wakilizuia gari la Joseph Mbilinyi kupita katika eneo hilo

Joseph Mbilinyi akiwasili eneo ambalo CCM wanafanyia mkutano na kukutana na umati wa wanaccm waliomzuia kupita


WATU 9 wamejeruhiwa na gari na pikipiki kuharuibiwa vibaya kutokana na vurugu zilizotokea baina ya wafuasi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA) na Chama cha Mapinduzi(CCM).

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Ahmed Msangi amethibitisha kutokea kwa tukio hilo  na kuongeza kuwa  lilitokea  juzi  majira ya saa kumi na moja jioni  eneo la Mbata – Buchani, Kata ya Ghana jijini hapa.

Alisema tukio hilo lilitokea wakati  mgombea ubunge Jimbo la Mbeya mjini kwa tiketi ya CCM, Sambwee Shitambala akiwa na wafuasi wake, wapenzi wa chama hicho alikuwa akifanya mkutano wa kampeni katika eneo hilo kwa mujibu wa ratiba yake.

Alisema mgombea huyo akiwa katika mkutano huo, mgombea ubunge jimbo la Mbeya mjini kwa tiketi ya Chadema Joseph Mbilinyi alikuwa akipita eneo hilo akiwa na msafara wake kuelekea maeneo ya Nsoho kwenye mkutano wa kampeni.

Kamanda Msangi alisema  kutokana na kitendo hicho wafuasi wa CCM ambao walionekana kuwa wengi hadi eneo la barabara hivyo kupelekea msafara wa Mbilinyi kutoweza kupita eneo hilo hali iliyopelekea kuzuka kwa vurugu zilizopelekea kujeruhiwa kwa watu na uharibifu wa mali.

Aliwataja majeruhi  wa vyama hivyo vya siasa kuwa ni  Robert Kerenge  (58) Katibu wa CCM Wilaya ya Mbeya, Salum Mwansasu (35) mkazi wa Majengo (CCM), Atupele Brown (39) mkazi wa Ghana (CCM), Rose Nelson (30) mkazi wa Majengo (CCM),Sakina Salum (25) mkazi wa Ghana (CCM), Malanyingi Matukuta (31) mkazi wa Forest (CCM), Agabo Mwakatobe (44) mkazi wa Ghana (CHADEMA), Jailos Mwaijande (23) mkazi wa Itiji (CHADEMA) na  Gabriel Mwaijande, dereva wa mgombea Ubunge (CHADEMA).


Kamanda Msangi aliongeza kuwa katika vurugu hizo gari la mgombea ubunge jimbo la Mbeya mjini kwa tiketi ya Chadema Joseph Mbilinyi aina ya Toyota land cruiser yenye namba za usajili T161 CPP liliharibiwa kioo cha mbele, taa moja ya nyuma upande wa kushoto na kioo cha upande wa dereva kwa kupigwa mawe.

Alisema  pia pikipiki zenye namba za usajili T332 CHV aina ya T-better na T383 CSE aina ya Skymark ziliharibiwa kwa kuvunjwa side mirror za upande wa kushoto na zipo kituo cha polisi kati.


Aliongeza kuwa kwa mujibu wa ratiba ya kampeni za uchaguzi iliyotolewa na Halmashauri ya Jiji la Mbeya kwa tarehe 17.09.2015, ilikuwa ikionyesha Chadema saa 4 asubuhi hadi saa 9 alasiri walitakiwa kufanya mkutano Kata ya Nsoho na saa 9 alasiri hadi 12 jioni walitakiwa kufanya mkutano Kata ya Maendeleo wakati Ccm kwa mujibu wa ratiba walitakiwa kufanya kampeni Kata ya Itende saa 2 asubuhi hadi saa 7 mchana na saa 7 mchana hadi saa 12 jioni mtaa wa Mbata, Kata ya Ghana ambapo tukio hili lilipotokea.


Alisema upelelezi unaendelea ikiwa ni pamoja na kupeleka jalada la uchunguzi kwa mwanasheria wa serikali ili waliohusika katika vurugu hizo wafikishwe mahakamani.

No comments: