Social Icons

Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com

bre

Monday, February 2, 2015

CHAMA CHA MAPINDUZI (CCM) MBEYA MJINI YAUNGANA NA WATANZANIA WOTE KUADHIMISHA MIAKA 38 YA KUZALIWA KWAKE.

Katibu wa CCM Mkoa wa Mbeya, Alhaji Mwangi Kundya, akiwahutubia wananchi wa Jiji la Mbeya katika sherehe za miaka 38 ya kuzaliwa CCM katika viwanja vya RuandaNzovwe.

Waendesha pikipiki wakiwa katika maandamano wakiingia katika uwanja wa shule ya Msingi Ruandanzovwe.

Meza kuu wakifuatilia kwa makini mambo yanayoendelea katika uwanja wa Shule ya Msingi Ruandanzovwe.

. Katibu wa CCM Wilaya ya Mbeya mjini, Kulwa Mironge, akiwatambulisha wageni mbali mbali waliohudhuria sherehe za miaka 38 ya kuzaliwa CCM.

 Mjumbe wa Mkutano Mkuu taifa Wilaya ya Mbeya mjini(MNEC) Sambwee Shitambala akimkabidhi fedha mtoto Anastazia(5) kwa ajili ya kuendea shule baada ya kuonesha juhudi katika kucheza mziki sambamba na baba yake Awilo.

Katibu wa Siasa Itikadi na Uenezi (CCM) Mbeya mjini, Philemon Mng'ong'o akimkaribisha Awilo kutoa burudani kwa wageni mbali mbali.

. Awilo akitoa burudani sambamba na mtoto wake.

Bendi ya Baby TOT ikiendelea kuwaburudisha wakazi wa Jiji la Mbeya.

Kikundi cha burudani cha Makhiri khiri kikitoa burudani.

. Ngoma ya asili ya Kinyakyusa maarufu kwa jina la Ling'oma kutoka Airport jijini Mbeya ikitumbuiza uwanjani.


Wananchi wakifuatilia kwa makini hotuba za viongozi.



CHAMA cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Mbeya mjini kimeadhimisha  miaka 38 tangu kuzaliwa kwa chama hicho kwa kuwakumbusha wananchi kujiandikisha katika daftari la kupigia kura.

Mjumbe wa Mkutano mkuu taifa kupitia Wilaya ya Mbeya mjini(MNEC) Sambwee Shitambala, alitoa wito huo katika sherehe zilizofanyika katika viwanja vya Shule ya Msingi Ruandanzovwe jijini Mbeya.

Shitambala alitumia nafasi hiyo kuwasihi Watanzania kujitokeza kwa wingi kujiandikisha kwenye daftari la kudumu la kupigia kura na kuhakikisha wanapata vitambulisho vitakavyosaidia wakati wa uchaguzi mkuu pamoja na kuipigia kura Katiba mpya.

Alisema vitambulisho vya sasa ni vizuri kutokana na kuwa vya kielektroniki ambavyo vitasaidia kuwadhibiti watu wasiowaaminifu ambao huwa na utaratibu wa kupiga kura mara mbili mbili kwa kuhamishwa eneo moja kwenda lingine.

Aidha Shitambala alitoa wito kwa wananchi kuacha tabia ya kupiga kura za potelea mbali kwa lengo la kuwakomesha baadhi ya wagombea kutokana na kuenguliwa kwenye kura za maoni kwamba tabia hiyo inaligharimu taifa kwani baadhi ya wanaochaguliwa wanakuwa hawana sifa ya kuongoza.

Alisema katika tathimini ya Viongozi waliochaguliwa katika Serikali za mitaa wengi wao ni miujiza tu kwani hawana uwezo wa kuongoza na hata kuelewa maana ya kuwa kiongozi hawaijui kutokana na kuchaguliwa kiholela baada ya wananchi kuchagua kwa kumkomesha mtu ama Chama.

Kwa upande wake Katibu wa CCM Mkoa wa Mbeya, Alhaji Mwangi Kundya ambaye alikuwa mgeni rasmi katika sherehe hizo, aliwashukuru Wananchi wa Mkoa wa Mbeya kwa kuipa CCM ushindi wa kishindo katika uchaguzi wa Serikali za mitaa uliofanyika Disemba 14, mwaka jana.

Kundya alisema kwa mtu mwenye akili timamu na katika mfumo wa vyama vingi vilivyoamua kuunganisha nguvu ili kushindana na Chama tawala lakini kimeshindwa kufikisha hata asilimia 20 ya kura zote ni wajibu kuwashukuru wananchi kwa kuendelea kuonesha imani kubwa kwa CCM.

Alisema vyama vingi vilianzishwa miaka 23 iliyopita lakini tangu hapo hawakuwahi kupata kiongozi yoyote hata ushindi mdogo katika chaguzi zilizopita ndiyo maana baada ya kuambulia viti hivyo vichache wakaona ni vema kukodi magari na kuanza kushangilia mitaani.

Katibu huyo aliongeza kuwa katika uchaguzi uliopita kwa Mkoa wa Mbeya CCM ilipata ushindi mkubwa tofauti na ilivyokuwa inatarajiwa kutokana na kuwepo kwa wabunge na madiwani wa Vyama vya upinzani kuwa wangesababisha kushindwa kupata matokeo mazuri.

Alisema Mkoa wa Mbeya wenye Vijiji 841 CCM imeshinda ngazi ya Uenyekiti katika vijiji 699 sawa na asilimia 83.12 huku vyama vyote vya upinzani vikigawana asilimia 16.88, kati ya Wajumbe 9195 CCM imepata wajumbe 7295 sawa na asilimia 83.62 na wapinzani wakipata wajumbe kwa asilimia 16.38.

Kundya aliongeza kuwa katika ngazi ya Wajumbe wa viti maalumu kwa Mkoa wa Mbeya walikuwa wagombea 5990 lakini CCM imepata wajumbe 5009 sawa na asilimia 83.62 na kuwaacha wapinzani wakiambulia asilimia 16.38, na kati ya Vitongoji 4445 CCM imepata vitongoji 3588 sawa na asilimia 80.72 na wapinzani wakiambulia asilimia 19.28 kati ya kura zote.

Katibu huyo aliongeza kuwa katika Halmashauri ya Jiji la Mbeya lenye mitaa 181 CCM ilipata Mitaa 107 sawa na asilimia 59.12 na vyama vya upinzani vikiambulia asilimia 40.88 na hii ni kutokana na kuwa na Mbunge pamoja na madiwani katika baadhi ya Kata.


Mwisho. 
Na Mbeya yetu

1 comment:

Anonymous said...

Kweli sherehe hii Mbeya haikuvutia kabisa. Uwanja wenyewe majani marefu inaonekana maandalizi hayakufanyika vya kutosha kama ilivyokuwa Songea. Uwanja huo kama ni muhimu kwa matukio maalum kwa nini haufanyiwi ukarabati ukawa katika hadhi nzuri. Yaani uko shaghalabaghala tu da! ndo CCm hiyo jamani