Social Icons

Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com

bre

Wednesday, April 16, 2014

MZAZI ATUHUMIWA KWA WIZI WA MTOTO WA SIKU TANO KYELA

MTUHUMIWA ANAETAFUTWA NA JESHI LA POLISI  KWA WIZI WA MTOTO

MAMA MZAZI WA MTOTO ALIYEIBIWA

BABA MZAZI ANAYETUHUMIWA KWA WIZI WA MTOTO



Jeshi la Polisi linamshikilia Salehe Issah Mwangosi(29) Mkazi wa Tankini Kasumulu Kata ya Itope Wilaya ya Kyela Mkoani Mbeya kwa tuhuma za wizi wa mtoto jinsi ya kiume mwenye umri wa  siku sita.

Imedaiwa kutenda kosa hilo dhidi ya mzazi mwenzake aliyefahamika kwa jina la Mboka Mwakikagile(21)mkazi wa Kitongoji cha Sama A Kijiji cha Ibanda Kata ya Itope Jumapili April 6 mwaka huu majira ya saa nne asubuhi kwa kushirikiana na mwanamke mmoja ambaye hajafahamika jina mara moja aliyejifanya ni mama yake mkubwa wa mtuhumiwa.

Mipango hiyo iliyoanza kuandaliwa na mtuhumiwa siku tatu baada ya mtoto kuzaliwa kwa kutumia simu ya kiganjani ya mtuhumiwa yenye namba 0767356222 na mzazi wa mtoto kwa namba 0757006839 ambapo siku ya tukio Salehe alimwambia kuwa mama yake mkubwa angekwenda kumjulia hali mtoto aliyezaliwa.

Baada ya Salehe kuwasiliana na mzazi mwenzake walikubaliana Mama yake mkubwa angekwenda Jumapili Aprili 6 mwaka huu majira ya saa nne asubuhi ambapo mwanamke huyo alifika nyumbani kwa Mboka(Mzazi wa mtoto)ambapo aliwakuta wazazi wake akiwemo Mzee Lupalo Elija Mwakikagile(90) na mkewe Nelly Kyusa(49) ambao walimpokea.

Mwanamke huyo alifikanyumbani kwa Mwakikagile akiwa ameshika mkoba wenye nguo za mtoto mchanga,sabuni na mahitaji mengine ambapo alijieleza kuwa yeye ni afisa wa Mamlaka ya mapato na Mama mkubwa wa Salehe hivyo amekuja kwa ajili ya kumjulia hali na kumpa pole Mboka kwa kujifungua.

Mama huyo baada ya kumwangalia Mtoto alidai ana matatizo ya macho hivyo waende naye Zahanati ya Njisi Kasumulu kwa ajili ya matibabu ambapo walipakizana kwenye pikipiki na kufika huko Zahanati na kumkuta Daktari ambaye alimtaka mzazi kununua Daftari ya matibabu kwa kuwa kadi ya kliniki hutolewa mwezi mmoja tangu kuzaliwa kwa mtoto.

Ndipo Mboka alikwenda Dukani umbali wa mita 500 kwa ajili ya kununua daftari akimwacha mwanamke huyo akiwa amembeba mtoto na aliporejea hakumkuta mwanamke huyo wa mtoto na hata aliposubiri kwa muda alimuuliza Salehe kupitia simu ya Daktari ambapo Salehe alisema asiwe na shaka mama huyo atamleta mtoto.

Mboka aliamua kutoa taarifa Polisi Kasumulu kwa ajili ya kuibiwa mtoto lakini alishangaa kumkuta Salehe Polisi naye akitoa taarifa juu ya kupotea kwa mtoto hali inayoonesha kulikuwa na njama kwani yeye ndiye alikuwa akifanya mawasiliano na mwanamke huyo na yeye ndiye aliyesema kuwa atakuja nyumbani kumwangalia.

Hata hivyo uchunguzi umebaini kuwa mwanake aliyedaiwa kuiba mtoto huyo alisajili upya namba ya simu badala ya awali kwa kutumia leseni yake ya udereva huku ikionesha kuwa amezaliwa April 24 mwaka 1986 na mara kadhaa alijitambulisha kama Afisa wa mamlaka ya mapato na wakati mwingine akijifanya Muuguzi.

Kwa upande wake ndugu wa mtuhumiwa akiwemo Baba mdogo aitwaye Assah Mwangosi(49)wamesema kuwa hawaelewi lolote kuhusiana na tukio hilo na kuwa hawakuwa na taarifa za kijana wao  kuzaa nje ya ndoa kwani Salehe ana mkewe aitwaye Falesy Sanderson(29) aliyemuoa mwaka 2006 alipokuwa akifanya biashara wilaya ya Karonga nchi jirani ya Malawi.

Ndugu wamedai Salehe anamiliki pikipiki mbili  zenye namba za usajili T640 CHA na T 796 BKG ambazo huzitumia kwa ajili ya kubeba abiria maarufu kama bodaboda eneo la Kasumulu na inasadikiwa moja ya pikipiki kutumika kuiba mtoto.

Kwa upande wa Jeshi la Polisi kupitia kwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya Ahmed Msangi amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba bado wanamshikilia Salehe kwa mahojiano na wanafanya juhudi za kumtafuta mtoto na kutoa wito kwa mwenye taarifa za mtoto huyo atoe Polisi na mtuhumiwa aweze kukamatwa.

Na Ezekiel Kamanga
Mbeya yetu

No comments: