Social Icons

Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com

bre

Monday, March 31, 2014

Mvua zasababisha kifo Chunya

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Ahmed Msangi 



MVUA zinazoendelea kunyesha sehemu mbali mbali hapa nchini zimesababisha madhara katika baadhi ya maeneo ikiwa ni pamoja na kusababisha vifo.

Mvua zilizonyesha Machi 30, Mwaka huu  Wilaya ya Chunya mkoani Mbeya zilisababisha kifo cha mtoto wa miaka minne baada ya kusombwa na maji ya mto uliojaa wakati akijaribu kuvuka akiwa na dada yake.

Marehemu alifahamika kwa jina la Vailet  Mwansopo(4)  na dada yake aliyenusurika kutokana na maji hayo ni Neva  Mwansopo(6) waliosombwa  na maji ya mto Hasano uliopo kitongoji cha Namalama kijiji cha Mpona Kata ya Totowe Wilayani hapa.

Watoto hao walikutwa na janga hilo walipokuwa wametoka nyumbani kwao Mpona kwenda kitongoji cha Hazolombo kinachotenganishwa na mto huo walikotumwa na Mama yao kwenda kumwita Baba yao mzazi Daimon Mwansopo ambaye anaishi na mke mwingine huko.

Kwa mujibu wa mashuhuda wa Tukio hilo, ambao ni Noel Mwazembe na Mlawa Mhamali walisema kuwa walisikia sauti ya kuomba msaada kwa mtoto Neva ndipo walipokimbilia eneo hilo na kuambiwa kuwa maji yalipomzidi nguvu aliamua kumwachia mdogo wake naye kufanya juhudi za kujiokoa ndipo walipofanikiwa kumwokoa Neva kisha kuanza kumfuatilia nduguye.

Walisema baada ya kufuatilia waliukuta mwili wa marehemu mita mia mbili kutoka eneo la tukio ukiwa umenasa kwenye mizizi ya miti kando kando ya mto huo ndipo walipouchukua kisha kutoa taarifa kwa Mtendaji wa kijiji cha Malangali Yaledi Mwanguku.

Walisema Mtendaji huyo  alitoa taarifa kituo cha Polisi Galula pamoja na  Daktari ambapo waliufanyia uchunguzi mwili wa marehemu na kuwabidhi ndugu kwa ajili ya mazishi.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Ahmed Msangi amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kutoa wito kwa wazazi kuwa waangalifu na watoto ili kuepusha vifo visivyo vya lazima.

Aliongeza kuwa Mvua zinazonyesha wilayani Chunya zimesababisha madhara makubwa ikiwemo uharibifu wa mazao na kuwataka wananchi kuwa waangarifu kwa kutozurura ovyo kutokana na mito mingi kujaa maji.

Mwisho.

No comments: