Social Icons

Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com

bre

Tuesday, October 29, 2013

WATU watano wameuawa kikatili katika matukio mawili tofauti yaliyotokea wilayani Chunya mkoani Mbeya likiwemo moja lililosababishwa na imani za kishirikina pamoja na wivu wa mapenzi.

Miili ya waliyochomwa moto kisa wivu wa mapenzi

Moja ya mwili wa aliyekuwa anatuhumiwa kwa mauwaji ya mzee Jampan nae aliuwawa na wananchi wenye hasira kali


Nyumbani kwa wapenzi waliochomwa moto kwa wivu wa mapenzi ndugu na majirani wakiomboleza


Chumba walicho jificha watuhumiwa wa mauwaji ya mzee Jampan watuhumiwa hao walianza kuptata kipigo kuanzia kwenye chumba hicho hadi mauti kuwakuta



Mwili wa mtuhumiwa mwingine wa pili ukiwa umelala huku wananchi wakitimua


Mwili wa  kikongwe na mkazi wa kijiji hicho Jampany Mhamali(78) ukiwa nje kusubiria polisi 




WATU watano wameuawa kikatili katika matukio mawili tofauti yaliyotokea wilayani Chunya mkoani Mbeya likiwemo moja lililosababishwa na imani za kishirikina pamoja  na  wivu wa mapenzi.

Tukio la kwanza lilitokea Oktoba 25 mwaka huu majira ya saa 2:00 usiku katika kijiji cha Mpona kata ya Totowe tarafa ya Songwe ambapo kikongwe na mkazi wa kijiji hicho Jampany Mhamali(78) akiwa njiani kurudi nyumbani akitokea kwenye kilabu cha pombe za kienyeji alivamiwa na watu wawili wasiofahamika na kukatwakatwa mapanga kichwani na mkono wake wa kulia hadi kufa.

Baada ya wakazi wa kijiji hicho kupata taarifa za mauaji hayo walijikusanya wakiwa na silaha za jadi ikiwemo mawe na kuanzisha msako mkali kwa kufuata nyayo za viatu vya watu waliotuhumiwa kuhusika na baadaye wakafanikiwa kuwakamata watu hao ambao hawakufahamika majina na kuanza kuwashushia kipigo na kuwaua wote wawili.

Watuhumiwa hao walikutwa kilomita kumi kutoka eneo la tukio wakiwa wamejifungia katika chumba namba tatu katika nyumba ya kulala wageni ya Hazole ilioko Malangali kata ya Totowe wakiwa wameficha mapanga chini ya godoro yanayohisiwa kutumika kwenye mauaji hayo.

Akizungumzia tukio hilo, Mtoto wa Marehemu January Mhamali alisema wauaji hao walifika nyumbani hapo siku tatu kabla ya tukio wakiwa na nia ya kuomba kazi ya kibarua cha kulima mashamba lakini marehemu alisema hana lakini wao waliendelea kufika kila siku huku wakipewa chakula.

Hata hivyo wakati wakiendelea kupigwa watuhumiwa hao walikiri kuhusika na mauaji ya kikongwe Mhamali na kueleza kuwa wao walitumwa na Maneno Adamson maarufu kwa jina la Lyambo ambaye alikuwa akimtuhumu kikongwe huyo kuwa ni mchawi.

Wanachi hao baada ya kuwaua watuhumiwa wawili walikwenda moja kwa moja nyumbani kwa mtuhumiwa wa tatu aliyetajwa kuwaagiza watu hao lakini kwa bahati mbaya hawakufanikiwa kumkuta kwani alikuwa amekwisha toroka.

Mujibu wa mhudumu wa nyumba ya kulala wageni Salome Emmanuel (26) alikiri kuwapokea wauaji hao na kwamba haikuwa mara ya kwanza kufika katika nyumba hiyo bali waliwahi kulala siku za nyuma na kusahau panga ambalo mhudumu aliwatunzia na kuwarudishia walipolihitaji.

 Alisema Siku ya tukio walitoka mapema katika chumba chao na kurejea majira ya saa nne usiku na kuongeza kuwa baada ya kufika walipata huduma ya vinywaji kabla ya kulala  na ndipo wananchi wakiongozwa na mtendaji wa Kijiji cha Malangali Yaredi Mwanguku walipofika na  kuwasihi wafungue mlango.

Hata hivyo Mtendaji huyo alipiga simu Polisi ambao walifika eneo la tukio wakiwa na silaha na kuwasihi wauaji hao kutoka nje lakini walikaidi amri ya Polisi ndipo wananchi zaidi ya 200 walipoamua kuvunja dirisha na kuanza kuwashambulia ambapo mmoja alifia papo hapo na mwingine kukimbia umbali wa kilomita moja kisha kukamatwa na kuuawa.

Wakati wananchi wakiwashambulia watu hao Askari Polisi aliyejulikana kwa jina la Zefa ambaye alikuwa akiwatuliza wananchi hao alijikuta katika wakati mgumu baada ya kupigwa jiwe kichwani ikiwa ni ishara ya kumwondoa katika eneo la tukio.


Aidha katika tukio la pili  Adelina Philimon(45) mkazi wa kijiji cha Magamba wilayani hapa na Wasiwasi Mwashiombo(28) mkazi wa kijiji cha Ipoloto Wilayani Mbozi waliuawa baada ya kuteketea kwa moto.

Wapenzi hao ambao kiumri ni sawa na mama na mtoto wake waliteketea kwa moto baada ya nyumba waliyokuwa wamelala kuchomwa moto na mtu aliyetajwa kwa jina la Zacharia Mwingila(39) mkazi wa Tunduma wilayani Momba.

Chanzo cha mauaji hayo ni wivu wa kimapenzi ambapo mtuhumiwa ambaye kwa sasa anashikiliwa na polisi alifikia hatua ya kuchoma moto nyumba baada ya kumkuta mpenzi wake akiwa amelala na mwanaume mwingine majira ya saa tano za usiku wa oktoba 25 mwaka huu katika kijiji cha Magamba wilayani Chunya.

Kwa mujibu wa mashuhuda wa tukio hilo  walisema mtuhumiwa huyo alianza kwa kuwachoma na visu wagoni wake na ndipo alipoamua kuchoma moto nyumba nzima ambayo iliwateketeza hadi kufa.

Kaimu kamanda wa polisi mkoani Mbeya, Robert Mayala alithibitisha kutokea kwa matukio hayo yote mawili na kuisihi jamii kuacha vitendo vya kujichukulia sheria mikononi na pia kuishi kwa kuwatuhumu wakazi wenzao wakiwahusisha na imani za kishirikina.

Ikiwa kuna Gazeti litatumia habari hii tuwasiliane kwa namba 
0654221465

Na Mbeya yetu

No comments: