Social Icons

Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com

bre

Friday, June 8, 2012

Shule Zageuka Sehemu Za Kazi Za Nyumbani



Wanafunzi wa shule ya Msingi Kising'a Isimani wakitumikishwa kuchota maji wakati wa masomo

Na Kenny Ngomuo,Mbeya (TGNP)
Wanawake na wanaume wa Kata ya Ijombe wilaya ya Mbeya vijijini mwishoni mwa wiki hii walitoa kilio chao katika warsha iliyoendeshwa na Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) katika kuchambua na kufuatilia kero mbalimbali wanazokumbana nazo katika eneo lao. Akizungumza kwa uchungu, Bi Siza Mistoni anasema shule ya Kata ya Iwalanje imekuwa mbali sana na makazi ( kilimeta zaidi sita toka kijiji cha Matanji) tatizo lililopelekea baadhi ya wanafunzi kutafuta vyumba vya kukodisha kwa jina maalum ‘GHETO’. … ‘Wanafunzi wamekuwa wakiishi kwenye magheto kwa muda mrefu na kupelekea wasichana wengi kutokufanya vizuri katika masomo yao kwani wao, wamegeuka kuwa wapishi , wanasaka maji, kuni kwa ajili ya kujipikia chakula. Kwa maana hiyo wasichana wamekuwa wakitumia muda wao mwingi zaidi kufanya kazi zilizo nje ya masomo tofauti wa watoto wa kiume ambao muda mwingi wamekuwa wakijisomea. Wasichana wengi wamepata mimba za utotoni na kuwapotezea ndoto zao za baadae. Wakazi hawa wamedai kuwa baadhi ya magheto wanayoishi wapo watoto wa kike na wakiume’, sambamba na hilo kuna uwezekano mkubwa na hatari ya kuongezeka kwa maambukiza ya magonjwa hatarishi kama vile Ukimwi.
Baadhi ya wanawake walioshiriki katika warsha ya uraghbishi wamewaasa wanawake na wanaume kuvuta nguvu za pamoja na kuwa mabalozi wa kuwafundisha watoto wao popote pale walipo kujua madhara ya mimba za utotoni. Wanafunzi waepuke tabia ya kubweteka kwa utandawazi ulioingia hapa nchini kwa kasi kubwa. Wanakijiji waliweza kuchambua mazuri ya utandawazi kama ukitumika vizuri ni njia mojawapo ya kujielimisha. Mfano wanafunzi wanaweza kupata taarifa sahihi kuhusiana na masomo yao, kuangalia taarifa za habari na kujua masuala mbalimbali yanayoendelea Tanzania, Afrika na Duniani kwa ujumla. Lakini wanafunzi hao hao wanatumia television kinyume na maadili kwa kuangalia picha za ngono .
Wanakijiji hawa wamebainisha pia kuwa kumekuwepo na ulevi wa kupindukia katika Kata ya Ijombe ambao unaathiri si tu maadili ya watoto bali hata wanaume ambao mara nyingi hupelekea kufanya ukatili wa kijinsia kwa wanawake na watoto wa kike. ‘ Mwanaume anakuja saa tano usiku anaaza kupiga kelele kudai chakula na anapokikosa kwa sababu hakuacha pesa matokeo yake ni kipigo kwa mwanamke’ alisema Bi Mage John wa kijiji cha Iwalanje.
Vile vile ilibainika kuwa wasichana wengi wanajiingiza katika vitendo viovu kwa kukosa msaada wa pesa kutoka kwa wazazi wao kwa ajili ya mahitaji yao shuleni kama chakula na vitabu.
Wanakijiji hao wameongeza kuwa shule za Kata zilizoanzishwa hazina walimu wa sayansi na vifaa vya maabara, kitendo kinachozima ndoto zao za baadae. Wakazi wa Kata ya Ijombe wamedai pia kuwa shule hizi zinachangisha pesa kila mwaka wanatoa elfu kumi ( 10,000/-) mbali na ada ya shilingi elfu ishirikini (20,000/=) kwa mwaka hawa ni wale wanaoishi nyumbani na kwenye magheto. Kwa wanafunzi wanaoishi mashuleni wanalipa laki nne na nusu (450,000/-kwa mwaka). Hata hivyo, wazazi hawa wamedai kuwa kuna michango mingine kama fedha za madawati, vitambulisho, bima za afya, tahadhari na rimu. Michango hii inakuwa ni kikwazo kwa wazazi ambao kipato chao ni kidogo. Wanawake pia wamedai kuwa mara nyingi mzigo wa kulipa ada unawaangukia wao kutokana na wanaume wengi kuwa walevi na kusahau familia zao.
Kwa upande wake mwanafunzi wa kidato cha nne Annety Bora anasema changamoto kubwa iliyopo katika shule ya Iwalanje ni ukosefu wa mabweni ya wasichana ambapo inapelekea baadhi ya wasichana kuishi kwenye madarasa kutokana na mabweni ya wasichana kutokuwepo shuleni hapo. Pia ameuomba uongozi wa shule uweze kufuatilia na kusimamia vyema uwepo wa walimu wa sayansi pamoja na vifaa vya kufundishia kwa ajili masomo ya sayansi kwani vilivyopo havikidhi mahitaji ya wanafunzi hao
Hata hivyo wananchi wanaolizunguka eneo la shule hiyo, wameuomba uongozi wa serikali katika ngazi ya Kata kuchukua hatua za haraka hasa kuhakikisha michango isiyokuwa ya lazima inaondolewa, kupata waalimu wenye sifa za kufundisha na siyo ‘yebo yebo’ na pia kulinda maadili na usalama wa watoto wetu.
Sigfred Peter Kimasa

No comments: