Social Icons

Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com

bre

Tuesday, May 3, 2016

MKUU WA MKOA WA MBEYA AMOS MAKALLA AOMBA USHIRIKIANO KWA WANAHABARI

Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Amos Makalla akiwa na Katibu Tawala wa Mkoa Mariam Mtunguja alipokutana na wanahabari wa mkoa wa Mbeya
 
Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Amos Mkalla akiwa na viongozi wa kitaifa wa Chama Cha Waandishi wa Habari za Utalii na Uwekezaji Tanzania(TAJATI) mara baada ya kikao chake na baadhi ya waandishi wa habari wa mkoa wa Mbeya kwenye ukumbi wa Mkapa jijini Mbeya


Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Amos Makalla akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wanahabari wa mkoa wa Mbeya kwenye ukumbi wa Mkapa 

Mkurugenzi wa Habari na Mahusiano wa TAJATI Felix Mwakyembe akizungumza jambo mbele ya mkuu wa mkoa wa Mbeya Amos Makalla kwenye ukumbi wa Mkapa
 
Mwenyekiti wa Kitaifa wa Chama Cha Waandishi wa Habari za Utalii na Uwekezaji Tanzania(TAJATI) Ulimboka Mwakilili akisisitiza jambo wakati wa kikao kilichomhusisha Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Amos Makalla na baadhi ya wanahabari wa mkoa wa Mbeya

Makamu Mwenyekiti wa TAJATI Christopher Nyenyembe akizungumza mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Amos Makalla kwenye ukumbi wa Mkapa
MKUU wa Mkoa wa Mbeya, Amos Makalla amewataka waandishi wa habari kuandika  habari zilizofanyiwa utafiti na  kweli zenye changamoto ili kuleta tija kwa jamii.
 
 
Makalla alitoa rai hiyo mwishoni mwa wiki katika kikao chake cha kujitambulisha kwa waandishi wa habari wa Mkoa wa Mbeya kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Mkapa uliopo jijini hapa.
 
 
Mkuu huyo wa Mkoa alisema ni vema Waandishi wa habari wakajilita katika kuibua habari za kweli na zenye changamoto zitakazoisadia serikali kuongoza na kutatua kero zinazoikabili jamii kwa ujumla.
 
 
Mbali na kutoa wito huo, Makalla aliomba ushirikiano wa kutosha kutoka kwa waandishi wa habari ili aweze kufanya kazi tofauti na mategemeo ya wengine wanaodhani anafanya siasa.
 
 
‘’Nataka wanasiasa wajue kuwa mie sifanyi siasa bali nimekuja kufanya kazi, najua wazi kuwa Jiji la Mbeya na halmashauri yake iko chini ya upinzani,wanasiasa wafanye siasa zao mie ninafanya kazi naomba ushirikiano wenu Waandishi,’’alisema Mkuu wa Mkoa.
 
 
Aliongeza kuwa uwezo wake wa kufanya kazi kwa kujituma na kutimiza wajibu wake unatokana na malezi mazuri aliyoyapata kutoka kwa wazazi wake ambao walimuusia kufanya kazi kwa bidii kupita malengo.
 
 
Alisema wapo baadhi ya wanasiasa wanabeza uongozi wake pamoja na utendaji kazi wake wakihusisha  na mambo ya siasa ingawa baadhi ya wanasiasa wanadhani utendaji wake unashinikizwa na kasi za kisiasa.
 
 
‘’Mie ni mtoto niliyekulia kwenye line za polisi, baba yangu na mama yangu walikuwa ni askari polisi, wote wameshatangulia mbele ya haki, Baba yangu aliniusia Nikipewa kazi nifanye kikweli kweli, na kiukweli ninapopewa kazi nafanya kazi kila nilipopewa majukumu huwa natimiza wajibu wangu i am serious nimekuja kufanya kazi sio siasa,’’alisisitiza.
 
 
Sanjari na azma yake hiyo ya kufanya kazi pia amewataka wanahabari kushiriki katika kuibua changamoto zilizopo ili ziweze kusukuma mbele maendeleo ya mkoa wa Mbeya katika nyanja za kiuchumi na kijamii.
 
 
Alisema wanahabari ni sekta muhimu inayoweza kuisaidia serikali katika kuibua mambo ya msingi ambayo yanaweza kuchukuliwa na kufanyiwa kazi na serikali.
 
 
Aidha Makalla ameelezea changamoto mbalimbali za utendaji zilizopo kwa watumishi wa umma huku akiweka bayana tatizo la watumishi hewa ambalo limeisababishia hasara serikali na kuwa amedhamiria kurejesha dhana ya utumishi bora kwa watumishi wa umma.
 
 
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi wa habari Mkoa wa Mbeya, Modest Nkulu alitoa wito kwa uongozi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya kujiepusha na vitendo vya kuwagawa waandishi hususani katika ziara mbali mbali.
 
 
Alisema ni kawaida viongozi wa Mkoa kubagua baadhi ya vyombo na waandishi jambo ambalo husababisha umoja wa waandishi kugawanyika na kukosa ushirikiano.
 
 

No comments: