Mkuu wa Wilaya ya Kyela Dk. Thea Ntara akisisitiza jambo alipokuwa akizungumza na wananchi katika operesheni ya kukagua usafi wa mazingira ili kukabiliana na ugonjwa wa kipindupindu |
Afisa Afya Wilaya ya Kyela, Geophrey Baroshi akionesha aina ya pombe zilizopigwa marufuku kutumiwa na watu hapa nchini ambazo zilikutwa katika maduka zikiuzwa wilayani Kyela. |
Mkuu wa Wilaya akisimamiazoezi la kukagua aina ya vinywaji vilivyopigwa marufuku kutumiwa nchini |
Baadhi ya Wananchi wakishiriki katika usafi wa mazingira |
Baadhi ya vialabu vya pombe za kienyeji vikivunjwa kutokana na kutokudhi vigezo ikiwemo ukosefu wa vyoo |
HALMASHAURI
ya Wilaya ya Kyela mkoani Mbeya imeweka utaratibu kwa wananchi wake kuhakikisha
wanaepukana na magonjwa ya kuambukiza hususani kipindupindu kwa kuwataka kila
kaya kujenga vyoo.
Kutokana
na agizo hilo Watu 17 wakazi wa Kijiji cha Lusungo Kata ya Lusungo wamekamatwa kwa kutokuwa na vyoo na uchafu wa
mazingira uliosababisha kuzorotesha
juhudi za kupambana na ugonjwa wa kipindupindu Wilayani humo.
Juhudi hizo
zimekuja baada ya ugonjwa huo kudumu kwa
kipindi cha miezi mitatu ambapo Kata ya Lusungo na Ndobo ndizo pekee ambazo bado
zina wagonjwa wa kipindupindu hali iliyomfanya Mkuu wa Wilaya ya Kyela Dk. Thea
Ntara kupiga kambi Kata ya Lusungo ili kufanya ukaguzi wa vyoo na usafi wa
mazingira.
Akizungumza
na gazeti hili katika ukaguzi huo, Mkuu wa Wilaya, Dk. Ntara alisema anakwamishwa
na Diwani wa Kata ya Lusungo Veronica Kanyanyila na Mwenyekiti wa Kijiji Zawadi
Lugano Mwangojola ambao wamekuwa wakidai ugonjwa huo umesababishwa na imani za
kishirikina na si uchafu au ukosefu wa vyoo.
Katika
oparesheni hiyo maalumu iliyofanywa na Mkuu wa Wilaya aliyeambatana na Maafisa
wa Afya pia iliyakumba maeneo mbalimbali kama Kata ya Ikama na Kijiji cha
Tenende ambapo alilazimika kuvunja Kilabu cha pombe Kata ya Ikama baada ya
kuwakuta wakazi wa eneo hilo wakinywa pombe za kienyeji katika mazingira
machafu.
Mbali
ya ukaguzi huo pia Mkuu wa Wilaya alishuhudia baadhi ya wananchi wakinywa pombe
ya moshi na pombe zilizopigwa marufuku kutoka nchi jirani na kulazimika
kuwakamata wahusika ambao wamefikishwa kituo kikuu cha Polisi Wilaya ya Kyela ambapo
pindi uchunguzi utakapokamilika watafikishwa mahakamani.
Pia Mkuu
huyo wa Wilaya aliteketeza sindano
zinazodhaniwa kutumika kwa ajili ya kujidunga na watumiaji wa madawa ya kulevya katika Kata ya Ikama na ambapo
alitoa agizo la kuwasaka wauzaji wa madawa hayo na wanaouza pombe zilizopigwa
marufuku kutoka nchi jirani.
Kwa
upande wake Afisa Afya Wilaya ya Kyela, Geophrey Baroshi alisema zoezi hilo ni endelevu na watahakikisha kila
kaya ina choo na kuwa na mazingira safi kwa muda wote ili kuutokomeza kabisa
ugonjwa huo Wilayani Kyela na kwamba waliokamatwa watafikishwa mahakamani
kujibu tuhuma zinazowakabili.
Mtendaji
wa Kijiji cha Lusungo Fadhili Sade alisema wamefanya ukaguzi katika kaya 681 za kijiji
hicho na zote hazina vyoo hali inayofanya mapambano ya kipindupindu kuwa magumu
mno kwani wengi wao wamekuwa wakiamini ugonjwa huo unatokana na ushirikina.
Naye Mtendaji
wa Kata ya Lusungo Stephen John alisema wamekuwa wakipokea vitisho kutoka kwa
Diwani wa Kata na Mwenyekiti wa kijiji kuwa aache kutangaza kuwa Kata hiyo
inakabiliwa na ugonjwa wa kipindupindu kwani ndiyo kunachochea kuongezeka kwa
ugonjwa huo ambao unatokana na ushikina na si uchafu au ukosefu wa vyoo.
No comments:
Post a Comment