Social Icons

Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com

bre

Wednesday, June 24, 2015

WASHAURI KUANZISHWA KWA GHALA LA KUTUNZIA VIFAA VYA MSAADA WA HARAKA MBEYA

Mganga mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Dk. Seif Mhina, mwenye shati la kitenge alipokuwa akichangia mada katika mafunzo yaliyotolewa na Redcross kwa Kamati ya Maafa na Majanga ya Mkoa wa Mbeya.

Mkurugenzi wa Maendeleo ya Mikoa na Matawi Redcross makao makuu, Julius Kejo, akitoa mada kwa viongozi wa kamati ya maafa Mkoa wa Mbeya katika mafunzo yaliyotolewa na Chama cha Msalaba mwekundu



Afisa Mahusiano wa Kamati ya kimataifa ya Redcross (ICRC) Nairobi Kenya, Viginia Njiru akiwasilisha mada kuhusu historia ya Redcross duniani pamoja na matumizi ya nembo zake.

Washiriki wa mafunzo wakifuatilia mada zinazowasilishwa.


 

KAMATI ya Maafa na Majanga Mkoa wa Mbeya imekishauri chama cha Msalaba mwekundu nchini(TRCS)kuanzisha ghala la kutunzia vifaa vya uokoaji na misaada ya dharula mkoani Mbeya.

Rai hiyo ilitolewa na Mganga mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Dk. Seif Mhina, alipokuwa akichangia mada katika mafunzo yaliyotolewa na Redcross kwa Kamati ya Maafa na Majanga ya Mkoa wa Mbeya.

Dk. Mhina alisema Mkoa wa Mbeya unamaeneo ambayo yamekuwa yakikumbwa na maafa mara kwa mara lakini juhudi za haraka za kuwafikia waathirika zinakwama kutokana na ukosefu wa msaada wa haraka.

Alisema ili kukabiliana na hali hiyo ni vema Chama cha Msalaba mwekundu kikaweka utaratibu wa kuwa na ghala la kuhifadhia vifaa vya uokoaji na misaada ya haraka mkoani Mbeya.

Alitolea mfano Wilaya ya Kyela kuwa imekuwa ikikumbwa na mafuriko mara kwa mara ambapo Kamati ya Maafa na majanga ya mkoa inakuwa haina msaada wa haraka wa kuwasaidia waathirika na wakiwasiliana na Redcross mkoa wa Mbeya wanasema msaada hadi utoke makao makuu jambo linalochelewesha upatikanaji wa misaada hiyo.

Aidha alisema uwepo wa ghala hilo kwa Mkoa wa Mbeya utasaidia pia kukabiliana na magonjwa ya milipuko inayoanzia nchi jirani kutokana na Mkoa huo kuwa mpakani.

“Mfikirie kuanzisha ghala kwa sababu ya mkoa wetu kuwa mpakani ili kuepukana na tishio la magonjwa kama ilivyokuwa Ebola, na kama tatizo ni ghala Serikali inalo na inaweza ikashirikiana na Redcross kuhifadhia  bidhaa husika” alishauri Mganga Mkuu.

Akijibu Changamoto hiyo, Mkurugenzi wa Maendeleo ya Matawi na Mikoa wa Redcross, Julius Kejo alipongeza kwa wazo na kujitolea kwa Ghala hilo na kuongeza kuwa Redcross wanautaratibu wake wa kuweka ghala mahali.

Alisema Redcross makao makuu wapo kwenye mchakato wa kuangalia namna watakavyoiwezesha ofisi ya Redcross mkoa wa Mbeya ili iweze kupatiwa ghala la kuhifadhia vifaa vya msaada wa dharula kwa waathirika wa majanga na maafa.

Aliongeza kuwa mchakato huo hautachukua muda mrefu kutokana na namna Chama cha Msalaba mwekundu Mkoa wa Mbeya kinavyoshiriki shughuli za kijamii na kuonesha ukomavu wake chini ya Mwenyekiti wake Ulimboka Mwakilili.

Aidha alitoa wito kwa Serikali kuipa mamlaka kamati ya Maafa na majanga ya Mkoa ili kufanya shughuli zake bila kuingiliwa kama ilivyo Mamlaka ya Udhibiti wa Chakula na dawa(TFDA).

Alisema Kamati hiyo ikiwa na mamlaka kamili itaweza kupanga mikakati namna ya kujiandaa na majanga kabla hayajatokea na kukabiliana pindi yatakapojitokeza bila kuchelewa.

Mwisho.


No comments: