Social Icons

Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com

bre

Thursday, October 16, 2014

KITUO CHA MSAADA WA KISHERIA CHUNYA CHAADHIMISHA KUMBUKUMBU YA KIFO CHA MWALIMU NYERERE KWA KUENDESHA WARSHA.

 Mkurugenzi mtendaji wa kituo cha msaada wa kisheria Chunya, Nyawili Kalenda akizungumza wakati wa warsha ya Wajibu na Haki.
 Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Chunya, Musa Wilbroad, ambaye alikuwa mgeni rasmi katika warsha hiyo akitoa hutuba ya ufunguzi.
 Mtoa mada katika warsha hiyo, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Chunya akiendelea kutoa mada katika Warsha hiyo kuhusu Haki na Wajibu.
 Mwenyekiti wa Warsha ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bakwata wilaya ya Chunya akiongoza warsha hiyo.
 Mkurugenzi mtendaji wa Kituo cha Msaada wa Kisheria Chunya, Nyawili Kalenda, akimkabidhi ripoti ya Kituo hicho kwa Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Chunya.
 Picha ya pamoja ya washiriki wa Warsha hiyo.



Washiriki wa Warsha wakifuatilia kwa makini.

 
KITUO cha msaada wa kisheria Chunya kimefanya maadhimisho ya  kumbukumbu ya kifo cha Mwalimu Nyerere kwa  kuendesha warsha na kufanya mkutano wake Mkuu.
 
Katika Warsha hiyo Kituo hicho (CHULECU) kimesema kimejipanga kuhakikisha kinafuatilia mwenendo wa uchaguzi wa serikali za mitaa sambamba na uchaguzi mkuu wa mwakani kwa Serikali na vyama vya Siasa kutojihusisha na rushwa.
 
Hayo yalibainishwa na Mkurugenzi mtendaji wa Chunya legal & Counselling unit(CHULECU), Nyawili Kalenda,  katika warsha iliyofanyika katika ukumbi wa Ofisi ya kijiji cha Mkwajuni wilayani Chunya mkoa wa Mbeya.
 
Katika warsha hiyo iliyokuwa na mada ya Wajibu na Haki iliyowashirikisha wananchi mbali mbali, viongozi wa dini,viongozi wa vyama vya siasa na viongozi wa mashirika yasiyokuwa ya kiserikali huku mtoa mada akiwa ni Hakimu Mkazi mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Chunya.
 
Kalenda aliwaambia washiriki kuwa Shirika lake ambalo ni Asasi isiyokuwa ya kiserikali itahakikisha uchaguzi wa serikali za mitaa pamoja na uchaguzi mkuu unafanyika pasipokuwa na viashiria vya rushwa pamoja na ukiukwaji wa sheria na haki za binadamu.
 
Alisema shirika limejipanga kufanya hivyo kama moja ya majukumu yake ambapo aliyataja majukumu mengine ya shirika lake ni pamoja na kutoa elimu ya uraia kwa jamii, kutoa msaada wa kisheria bure, kutoa ushauri nasihi,kufanya utafiti wa maswala ya kisheria yanayovunjwa na utunzaji wa mazingira.
 
Alizitaja shughuli zingine kuwa ni kufanya uangalizi wa vyombo vinavyotoa maamuzi kama mabaraza ya ushauri ya vijiji na kata, Mahakama na vituo vua usuluhishi na kuchapisha machapisho ya sheria kwa lugha inayoweza kueleweka kwa kila mwananchi.
 
Kwa upande wake mgeni rasmi aliyekuwa akizindua Warsha hiyo, Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Chunya, Musa Wilbroad, ambaye pia ni Afisa Tarafa ya Kwimba, alisema vituo vya Sheria visivyokuwa vya kiserikali vinapaswa kufanya kazi zaidi vijijini.
 
Alisema wananchi waishio vijijini wanateseka sana na kuonewa katika maswala ya kisheria kutokana na kutojua njia za kufuata ili wapate haki hivyo ni jukumu la Asasi hizo kujikita vijijini ili kuwasaidia wananchi na sio kukaa maofisini kusubiria mashauriano.
 
Naye Mtoa mada katika Warsha hiyo, Hakimu Mkazi mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Chunya,Othmund Ngatunga akisaidiwa na mwanasheria wa Halmashauri ya Wilaya ya Chunya, Twavusitile Simanyani, walisema suala linalosumbua jamii ni wananchi kutojua sehemu ya kupeleka malalamiko yao.
 
Walisema mara nyingi malalamiko yanayohusu migogoro ya ardhi wengi wao hukimbilia kituo cha polisi ama Mahakamani jambo linalopelekea kuchelewa kupatikana kwa haki na kulundika kesi zisizokuwa na  msingi sehemu isiyohusika.
 
Walisema ili hayo yote yaishe ni kazi ya vituo vya sheria kutoa elimu kwa wananchi kuhusu sehemu sahihi ambako wanaweza kupeleka malalamiko yao na yakapatiwa ufumbuzi bila milolongo yoyote.
Baadhi ya washiriki wa warsha hiyo walitoa ushauri kwa Mahakama kufanya utaratibu wa kuzunguka vijijini na kutoa elimu juu ya sheria kupitia mikutano ya hadhara ili kuwaondolea mkanganyiko wananchi pindi wanapohukumiwa.
 
Kutokana na ushauri huo, Hakimu Ngatunga alipinga suala hilo na kwamba mwenye wajibu wa kuzunguka na kutoa elimu ni mbune na diwani ambao ndiyo wanaotunga sheria na kwamba kazi ya Mahakama ni kutafsiri sheria kutoa haki.

Na Mbeya yetu

No comments: