Social Icons

Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com

bre

Tuesday, January 28, 2014

USHAHIDI wa kesi inayowakabili Askari Polisi mmoja na Askari Magereza pamoja na Raia wengine watatu wanaotuhumiwa kwa unyang’anyi wa kutumia nguvu umeendelea kutolewa katika Mahakama ya Wilaya ya Mbeya.











USHAHIDI wa kesi inayowakabili Askari Polisi mmoja na Askari Magereza pamoja na Raia wengine watatu wanaotuhumiwa kwa unyang’anyi wa kutumia nguvu umeendelea kutolewa katika Mahakama ya Wilaya ya Mbeya.

Katika Kesi hiyo, Mhakama iliweza kusikiliza ushahidi wa Shahidi mmoja tofauti na Mashahidi Sita kama upande wa Waendesha mashtaka ulivyodai mbele ya Mahakama ya Wilaya ya Mbeya chini ya Hakimu Mfawidhi, Michael Mteite.

Shahidi huyo ambaye ni shahidi namba mbili kwa mujibu wa Mahakama, Kitinkwi Mtatiro ambaye ni Mkaguzi msaidizi wa Polisi na Mkuu wa Kitengo cha Upelelezi (O-CID) Wilaya ya Mbeya, ambaye aliiambia Mahakama kuwa siku ya ambayo ni Januari 3, Mwaka huu alikuwa kwenye majukumu yake ya kazi ya kila Siku.

Shahidi huyo ambaye alikuwa akiongozwa na Mwendesha Mashtaka wa Serikali, Basilius Namkambe, alisema majukumu yake ya kila siku ni pamoja na kuangalia nidhamu ya Askari waliochini yake, kufuatilia makosa makubwa pamoja na kufanya kazi za upekuzi maeneo mbali mbali.

Alisema siku ya tukio alimuaga bosi wake ambaye ni Mkuu wa Polisi Wilaya ya Mbeya kuwa anaenda kufuatilia tukio la uhalifu maeneo ya Soweto ambapo baada ya kufika huko muda mfupi tu alipokea simu kutoka kwa Bosi wake huyo huyo akimweleza kuwa amepata taarifa kutoka kwa msamaria mwema kuwa kuna tukio la uporaji eneo la Kawetere.

Shahidi huyo aliendelea kuieleza Mahakama kuwa baada ya kupokea maelezo hayo aliwasiliana na Msaidizi wake aliyemtaja kwa jina la Philibert Matoo ambaye alienda eneo la tukio huku wakiendelea kuwasiliana kupitia Simu ya upepo(Redio call).

Alisema wakati akisikia maelekezo kupitia simu ya upepo alisikia Msaidizi wake akiomba msaada wa nguvu kisha mawasiliano yakakatika na kumlazimu yeye mwenyewe kuacha kazi aliyokuwa akiifanya na kuamua kuelekea eneo la tukio.

Alisema alipokuwa njiani kuelekea eneo la tukio akiwa Isanga tankini alikutana na msafara wa magari matano yakiwa yanakimbia ambapo aliweza kuligundua gari la polisi aina ya Landcruser ndipo alipoamua kuunga msafara ulioishia katika kituo cha Polisi cha Kati.

Alisema baada ya kufikia eneo hilo alipewa maelekezo kutoka kwa msaidizi wake ambapo baada ya hapo aliandaa hati ya dharula ya kupekua mali wazokuwa nazo kwenye magari mawili yaliyokuwa yakimikiwa na watuhumiwa.

Alisema kwenye gari ya Kwanza yenye namba za Chesesi  GX 6011832 Aina ya Grand Mark II, iliyokuwa ikiendeshwa na mtuhumiwa namba moja ambaye ni PC James mwenye namba F8302 akiwa na mtuhumiwa namba tatu,walikuta mabegi mawili ya nguo, Laptop Mbili, Chaji ya Simu,Simu mbili za Mkononi pamoja na Pingu moja.

Aliongeza kuwa katika upekuzi katika Gari ya pili aina ya Toyota Cresta yenye namba T 182 BEU Mali ya mtuhumiwa namba mbili Elinazi Mshana na kukuta Mablanketi mawili yakiwa kwenye mifuko yake.

Hata hivyo Mwendesha Mashtaka wa Serikali aliiomba Mahakama kupokea maelezo ya upekuzi kama vielelezo vitakavyotumiwa na mahakama jambo amblo lilipingwa vikali na upande wa utetezi ukiongozwa na Wakili Ladislaus Lwekaza ambaye alidai kuwa maelezo hayo hayakuandikwa katika katatasi maalumu kwa mujibu wa kifungu cha 38.

Akijibu pingamizi hilo, Namkambe alisema Shahidi wake alisema alifanya upekuzi katika mazingira ya dharula kwa mujibu wa kifungu cha 42 na siyo anavyodai wakili wa utetezi.

Kutokana na majibizano hayo Mahakama ilipokea maelezo hayo kama kielelezo P2 ambapo pia Mahakama ililazimika kuhamia Nje kwa ajili ya Shahidi kutambua magari waliyokutwa nayo watuhumiwa ambapo baada ya kutambuliwa pamoja na vitu vilivyokutwa yalipokelewa kama vielelezo kama P3 na P4.

Awali Mwendesha mashtaka wa Serikali Basilius Namkambe alisema washtakiwa wote kwa pamoja  wanatuhumiwa kwa kosa moja la unyang’anyi  kinyume cha Sheria kifungu cha 287 sura ya 16 kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.

 Namkambe  aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Mshitakiwa namba moja ambaye ni Askari Polisi PC James mwenye namba F8302 wa Wilaya ya Mbeya ambaye kabla ya kufikishwa mahakamani alivuliwa Uaskari baada ya kuhukumiwa kijeshi.

Aliwataja wengine kuwa ni mshtakiwa namba mbili kuwa ni Elinanzi Mshana(22)Mkazi wa Iyela Jijini Mbeya, Askari Magereza mwenye namba B 500 Sajenti Juma Mussa(37) wa Gereza la Ruanda Mbeya,Mbaruku Hamis(29) Mkazi wa Iyela na Amri Kihenya(38) Mkazi wa Iyela.

Akisoma mashtaka yao Mbele ya Hakimu Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Michael Mteite, Namkambe alisema watuhumiwa hao walitenda kosa hilo Januari 3, Mwaka huu majira ya saa 11 jioni katika eneo la Mlima Kawetere barabara ya Mbeya Chunya.

Alisema watuhumiwa hao kwa pamoja walitenda kosa hilo kwa kulizuia gari aina ya Pick Up lililokuwa likiendeshwa na Ezekia Matatira (34) Mkazi wa Iyunga Jijini Mbeya ambaye alikuwa na mtu aliyekuwa akifahamika kwa jina la Sreedhar Pasupelet(38) mwenye asili ya Kiasia wakitumia magari madogo mawili ambayo ni GX 100 Toyota Cresta T 782 BEU na Gari linguine ambalo lilikuwa na namba za Chesesi GX 6011832 AINA YA Grand Mark II.

Kesi hiyo imeahirishwa hadi kesho kwa mashahidi wengine kuendelea kutoa ushahidi wao, huku Mahakama hiyo ikiendelea kusisitiza kuwa itahakikisha kuwa kesi hiyo itaisha muda mfupi kama ilivyopangwa.

Na Mbeya yetu


No comments: