Mratibu wa Magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele kutoka Wizara ya Afya, Dk. Upendo Mwingira akifafanua jambo katika semina ya waandishi wa habari Mkoa wa Mbeya kuhusiana na magonjwa hayo. |
Baadhi ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Mbeya wakifuatilia Semina kuhusu Magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele. |
IMEELEZWA kuwa chanzo cha
kuongezeka kwa magonjwa ambayo yalikuwa
hayapewi kipaumbele kimetokana na imani potofu na umaskini miongoni mwa jamii hali
iliyopelekea kushindwa kupata matibabu kwa wakati.
Hayo yalibainishwa na
Mratibu wa Magonjwa ambayo yalikuwa hayapewi kipaumbele wa Wizara ya Afya,
jinsia, maendeleo ya jamii, wazee na watoto, Dk. Upendo Mwingira wakati wa
mafunzo kwa waandishi wa habari wa Mkoa wa Mbeya na Songwe yaliyofanyika katika
ukumbi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mbeya.
Dk. Mwingira alisema jamii
nyingi iliyachukulia magonjwa hayo kama suala la kiimani na kwamba haikujua
kama matibabu yapo na mgonjwa huweza kupona kabisa ambapo pia elimu ndogo na
umaskini unachangia kutotambua namna ya kukabiliana nayo.
Aliyataja magonjwa hayo kuwa ni
Usubi unaosababishwa na minyoo inayoenezwa na inzi weusi, Matende na Mabusha
yanayoenezwa na mbu aina ya culex na Anopheles, Trakoma inayosababishwa na bacteria,Kichocho
kinachosababishwa na konokono pamoja na ugonjwa wa minyoo ya tumbo.
Alisema magonjwa hayo
yanapatikana zaidi katika mikoa ya ukanda wa Pwani ambapo utafiti umeonesha
kuyakumba maeneo mengine ya Nchi ambapo alisema magonjwa mengine ni Malale,
Kichaa cha Mbwa,Tegu, Bruceloza na ugonjwa wa Tauni.
Aliongeza kuwa mkakati wa
Serikali ni kuhakikisha inahamasisha jamii ya Watanzania walioathirika na
magonjwa hayo pamoja na wengine wanatumia dawa za kinga tiba bila kujali kama
amepata maambukizi au hajapata ili baadhi ya magonjwa kuyadhibiti na mengine
kuyatokomeza kabisa hadi ifikapo 2020.
Alisema zoezi la kugawa daza za
kingatiba limeshaanza kwa baadhi ya mikoa ambapo asilimia kubwa ya dozi ni
mwaka mmoja na kwamba dawa hizo zitatolewa bure kwa kila mwananchi kupitia kila
kaya au vituo vya afya na zahanati.
Akizungumzia malengo ya mafunzo
hayo kwa waandishi wa habari, Dk. Mwingira alisema ni kufikisha ujumbe kwa
jamii kwa haraka juu ya magonjwa ambayo yalikuwa hayapewi kipaumbele ili
wananchi wapate elimu na kutumia dawa za kinga tiba.
Aliongeza kuwa lengo linguine ni
kuwawezesha wanahabari kuelewa undani juu ya mpango wa kudhibiti na
kuyatokomeza magonjwa hayo, kuwawezesha kutoa elimu kwa jamii na kuwajengea
uwezo na uelewa kwa jamii kuhusiana na faida ya dawa zenye kingatiba.
No comments:
Post a Comment