Social Icons

Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com

bre

Friday, October 23, 2015

SHIRIKISHO LA WASOMI NA VYAMA VYA SIASA MKOA WA MBEYA WAMUUNGA MKONO DK. MAGUFULI.

 
Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyama vya siasa Mkoa wa Mbeya, Godfrey Mwandulusya ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha APPT - Maendeleo Mkoa wa Mbeya akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na uchaguzi unaotarajiwa kufanyika hivi karibuni.

Mwenyekiti wa Shirikisho la Wasomi Mkoa wa Mbeya, Prince Mwaihojo akifafanua jambo kwa waandishi wa habari kuhusu kiongozi anayekubalika katika jamii.

Viongozi wa Mashirikisho wakiwa kwenye mkutano na waandishi wa habari.



Baadhi ya Waandishi wa Habari wakiwa kwenye mkutano na wenyeviti wa Mashirikisho Mkoa wa Mbeya.

ZIKIWA zimebaki  siku mbili kuelekea uchaguzi mkuu wa Tanzania, Shirikisho la Vyama vya siasa na Shirikisho la Wasomi Mkoa wa Mbeya kwa pamoja wamesema wanamuunga mkono mgombea Urais kwa tiketi ya Chama cha Mapinduzi (CCM) Dk. John Magufuli kwa madai kuwa ni mtendaji mzuri.
 
Wakizungumza katika mkutano na waandishi wa habari uliofanyika katika ukumbi wa Hotel ya Mbeya Peak, Viongozi wa mashirikisho hayo walisema Dk. Magufuli anakipaji cha utendaji sio wa kufundishwa ni tofauti na wagombea wengine.
 
Mwenyekiti wa Shirikisho la Wasomi Mkoa wa Mbeya, Prince Mwaihojo, alisema Dk. Magufuli anaweza kukemea jambo baya linapotokea na sio mtu wa kusubiri maovu yakatendeka na kwamba utendaji wake amezaliwa nao.
 
Alisema Wagombea wengine wanahubiri siasa za mitaani ambazo haziwezi kuwasaidia watanzania kwa ujumla kwani wamejikita zaidi kwenye kundi la Boda boda lengo lao likiwa ni kuwatumia katika vurugu kwani wanajua hawawezi kushinda katika uchaguzi huo.
 
Alisema hivi sasa Watanzania wanapaswa kumuangalia mtu anayeweza kuwaongoza na sio kuangalia Chama anachotoka ndiyo maana Shirikisho hilo limeanzisha msemo wa Mbeya kwanza vyama baadaye ili kumpata kiongozi anayefaa bila kujali itikadi yake.
 
“Sisi Wasomi wa Mkoa wa Mbeya tumeona tusimamie kwenye mtu anayefaa kwa maslahi ya Watanzania wote bila kujali chama anachotokea hivyo tunamuunga Mkono Dk. Magufuli kwa kuwa ni mtendaji mzuri mwenye kipaji na mwenye uwezo wa kutatua changamoto katika jamii” alisema Mwaihojo.
 
Alisema wagombea wengine wanashindwa kusimamia kauli wanazotoa badala yake wamekuwa vigeu geu kwa kushindwa kukumbuka kile walichokiongea mbele ya hadhara na badala yake wamekuwa wakitoa kauli zinazokinzana.
 
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyama vya siasa Mkoa wa Mbeya na Mwenyekiti wa  APPT Maendeleo Mkoa wa Mbeya, Godfrey Mwandulusya, ametoa wito kwa vijana kutokubali kutumiwa vibaya na baadhi ya viongozi wa siasa katika kulinda kura jambo ambalo ni kinyume cha sheria za uchaguzi.
 
 Alisema kitendo hicho kinaashiria vurugu na kuharibu taswira ya uchaguzi na kwamba maagizo ya Tume ya uchaguzi ya kuwataka wapiga kura kusimama mita 200 yako sahihi kwa  kuwa sheria mama inatamka wazi kuwa kusanyiko lolote la kuanzia watu watatu ni kosa kisheria.
 
Alisema ni vema wakazi wa Mbeya wakaheshimu maagizo ya Tume kwa kupiga kura kasha kurudi nyumbani kwa kuwa vyama vya siasa vitaweka mawakala wao ambao jukumu lao ni kulinda kura wakati wa uchaguzi.
 
Aliongeza kuwa vurugu zinazotokea Mkoa wa Mbeya zinakosesha fursa za ajira na kukimbia kwa wawekezaji kwenye sekta za viwanda hivyo ni vema vijana wakakataa kutumiwa na baadhi ya viongozi kwa manufaa yao binafsi.
 
“ Shirikisho la vyama vya siasa Mkoa wa Mbeya nje ya Ukawa inawataka vijana kupiga kura na kurudi nyumbani, hao wagombea wanaowataka walinde kura wao watakuwa wapi kuzilinda hizo kura zao hadi wawaachie vijana? Hawaoni kama wanawatumia kutaka kuleta vurugu” alihoji Mwandulusya.

No comments: