Social Icons

Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com

bre

Monday, March 17, 2014

WALIOSHINDA TUZO ZA EJAT KUTOKA MBEYA WAPONGEZWA

Rashidi Mkwinda aliyeshika nafasi ya pili katika kipengere cha Uandishi wa Habari za Mazingira.


Festo Sikagonamo nafasi ya pili katika Kipengere cha Uandishi wa Habari za Utawala


Gordon Kalulunga aliyeshinda katika kipengere cha Uandishi wa Habari za Afya na Uzazi.




MTANDAO wa Kijamii wa www.mbeyayetu.blogspot.com na Kampuni nzima ya Tone Multimedia Company Limited(TMCL) unawapongeza waandishi wa Habari walioibuka kidedea katika kinyang’anyiro cha umahiri wa uandishi wa Habari (EJAT) zilizoandaliwa na Baraza la Habari Tanzania(MCT).

Mbali na kuwapongeza waandishi wa Nchi nzima waliobahatika kuchaguliwa kushiriki kinyang’anyiro hicho na wengine kuchaguliwa katika nafasi mbali mbali Mtandao huu unawapongeza wawakilishi wa Mkoa wa Mbeya katika Tuzo hizo kwa kuibuka washindi katika Fainali iliyofanyika katika Ukumbi wa Mlimani City Jijini Dar Es Salaam.

Waandishi hao ni pamoja na Rashidi Mkwinda aliyeshika nafasi ya pili katika kipengere cha Uandishi wa Habari za Mazingira, Festo Sikagonamo nafasi ya pili katika Kipengere cha Uandishi wa Habari za Utawala Bora sambamba na Gordon Kalulunga aliyeshinda katika kipengere cha Uandishi wa Habari za Afya na Uzazi.

Washindi hao waliowakilisha vema Mkoa wa Mbeya kwa pamoja walitunukiwa Vyeti, Ving’amuzi pamoja na madishi ya DSTV kila mmoja.

Mtandao huu unatoa pongezi na wito kwa wanahabari wengine kuiga mfano wa kujituma katika kuandika habari za kijamii ili hatimaye na wao waje kuibuka washindi katika mashindano yajao ili kuboresha utendaji kazi na weledi wa taaluma ya habari katika Mkoa wetu wa Mbeya.

Aidha baadhi ya Wadau wa Habari Mkoani hapa ambao hawakutaka kuandikwa majina yao walitofautiana kuhusu utaratibu unaotumika kuwapata washindi ambapo baadhi yao walipongeza na wengine wakiponda kwa madai kuwa utaratibu huo umepitwa na wakati na kwamba wahusika wanapaswa kubadilika.

Walisema kawaida mtu hawezi kuomba kupewa au kuchaguliwa kuwa mshindi katika nafasi yoyote isipokuwa ni kwa wadau wanaofuatilia habari hizo ndiyo wanaoweza kuchagua ama kumteua mfanyakazi bora na mahiri wa uandishi kutokana na mguso wa habari anazoziandika.

Waliotolea mfano namna anavyopatikana mfanyakazi bora katika taasisi katika kilele cha siku ya wafanyakazi duniani kuwa hupigiwa kura na wafanyakazi wenzie na siyo wao kupeleka maombi na kuongeza kuwa hata katika kumpata mchezaji bora pia hupigiwa kura na mashabiki na sio wachezaji kutuma maombi.

Walisema suala hilo linaweza kuwa na viashiria vya rushwa kwa baadhi ya washiriki kutaka kujaribukuwashawishi wahusika ili wawachague kuwa washindi kutokana na utaratibu unaotumika kutoenda na wakati.

Walienda mbali zaidi kuwa pia mitandao ya kijamii inapaswa kuhusishwa katika vinyang’anyiro hivyo kwa kuwa ndicho chanzo cha habari zinazochapishwa kwenye baadhi ya magazeti na vituo vya Redio ambavyo huombea tuzo habari walizozitoa kwenye mitandao.

Mwisho.

Na Mbeya yetu


No comments: