Social Icons

Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com

bre

Wednesday, August 22, 2012

WAKULIMA WATAKIWA KUTUMIA VYEMA ELIMU WALIYOPATA MAONESHO YA NANE NANE




BAADA ya maonesho ya Wakulima (Nanenane) kufikia kilele Agosti 8, Mwaka huu baadhi ya wadau wa sekta ya kilimo Mkoani Mbeya wameanza kutoa maoni yano kutokana na tathimini ya maonesho yalivyokuwa.

Aidha wakulima wa Mikoa ya Kanda ya Nyanda za Juu kusini wametakiwa kutumia vyema elimu wanayoipata katika sherehe za Maonesho hayo na  kutafsiri kiuhalisia katika shughuli zao za kilimo kwa lengo la kuongeza thamani ya mazao yao .

Pia wadau hao wamewatupia lawama Maofisa Ugani kwa kuitokuwa wabunifu badala yake kuendeleza teknolojia za kilimo na mifugo zilizopitwa na wakati ambazo hazimsaidii mkulima kuendana na soko la ushindani.

Pamoja na hayo  wakulima  wamehimizwa kuondokana na kilimo cha mazoea badala yake watumie maonesho hayo kwa kujifunza na kuelewa namna ya kuanzisha kilimo bora kwa kufuata ushauri wa wataalamu wa kilimo katika maeneo yao pamoja na kuhakikisha  wanaungana kwa makundi  ili kuongeza uzalishaji na kuwasaidia kupata soko la uhakika ndani na na nje ya nchi.

Mmoja wa wadau wa kilimo Mkoani Mbeya,Akizungumzia mafanikio na changamoto zinazowakabili wakulima wa mikoa hiyo hasa katika sherehe za wakulima nanenane wakati akifanya mahojiano maalumu na gazeti hili, Mwenyekiti wa Wafanyabiashara  Mkoani hapa Julius Kaijage alisema wakulima wa mikoa hiyo bado wanakabiliwa na changamoto nyingi licha ya halimashauri zao kuwawezesha kushiriki maonesho  hayo kwa gharama nyingi.

Alisema  umefika wakati kwa wakulima hao wakaondokana na mtazamo kuwa maonesho ya nanenane kuwa  ndio sehemu pekee ya kuonyesha mbinu za uzalishaji wa mazao katika maeneo yao badala yake waende kwenye uhalisia wenyewe.

Aliongeza kuwa asilimia kubwa ya mabanda yaliyoko katika maonesho hayo yamekuwa yakionyesha namna ambavyo wakulima walivyo weza kufikia malengo ya uzalishaji wa kisasa lakini imekuwa tofauti na uhalisia wenyewe kama wanavyo jieleza kwenye mabanda hayo.

Kaijage alisema ni vema sasa viongozi na wataalamu kwa ujumla wakatafakari namna ya kumpatia elimu mkulima ambayo itaweza kumsadia katika shughuli zake za kilimo  badala ya kusubiri maonyesho kwani kutasaidia pia kukuza na kuongeza thamani ya mazao.

Alisema mara baada ya maonesho hayo kufikia kilele kunatakiwa kuwepo na mabadiliko kwa wakulima wenyewe kutokana na elimu iliyopatikana kwenye maonyesho hayo.

Aidha mwenyekiti huyo amewataka wakulima hao pia kuungana kwa pamoja ili kupata soko la uhakika ndani na nje ya nchi kwa lengo la kuinua kipato chao.

Katika hatua nyingine Mdau mwingine aliyejitambulisha kwa jina moja la Kunzugala  aliwataka maafisa ugani katika mikoa hiyo kutoa elimu ya kilimo bora kwa wakulima moja kwa moja katika maeneo yao badala ya kukaa maofisini wakisubiri taarifa.

Alitanabaisha kuwa tatizo kubwa la maofisa kilimo wengi wamekuwa wakishinda maofisini badala ya kwenda kwa wakulima  kutoa elimu hali inayochangia kudidimia kwa sekta ya kilimo kwa asilimia kubwa kitendo ambacho kinawafanya wakulima wengi kutotumia   kanuni bora za kilimo kutokana na kukosa uelewa.

Kwa hisani ya Venance Matinya, Mbeya. 


No comments: