26/7/2011SERIKALI  imewataka viongozi wa Mchezo wa Pool table nchini kuwaelekeza wachezaji  wao ili wajue muda muafaka wa kuchezwa kwa mchezo huo jambo ambalo  litawafanya waachane na tabia ya kucheza wakati wa kazi.
Wito  huo umetolewa jana na waziri wa Nishati na Madini William Ngeleja  wakati akikabidhi zawadi kwa wabunge washindi wa mchezo huo zilitotolewa  na Chama Cha Pool Tanzania (TAPA) katika hafla fupi iliyofanyika nje ya  viwanja vya Bunge mjini Dodoma.
Waziri  Ngeleja alisema kuwa hivi sasa mchezo huo umekuwa ukichezwa muda wowote  hasa wakati wa kazi jambo ambalo limewafanya viongozi na baadhi ya  wananchi  kuulalamikia kuwa unapoteza nguvu kazi ya taifa.
 “Nawaomba  mfikishe ujumbe kwa wachezaji na mashabiki wenu ili wajue muda muafaka  na kupanga ratiba ya kucheza Pool table na si kucheza muda wowote hasa  wakati wa kazi  na hivyo kupoteza nguvu kazi ya taifa”, Ngeleja akiwaambia viongozi wa TAPA .
Naye Kapteni wa timu  ya  Bunge Idd Azan ambaye ni Mbunge wa Kinondoni aliwapongeza viongozi wa  chama hicho kwa jitihada wanazozifanya za kuutangaza mchezo huo na  kuahidi kuwapa ushirikiano zaidi. 
Kwa  upande wake Mwenyekiti wa Chama hicho Isaack Togocho alisema kuwa  anafurahi kuona kuwa wabunge wameupokea kwa moyo mkunjufu mchezo huo na  anaamini kuwa watakuwa  mabalozi wao wazuri . 
Waliokabidhiwa zawadi ni mshindi wa jumla wa mashindano hayo George Simbachawene ambaye ni Mbunge wa  Kibakwe alikabidhiwa zawadi ya ngao na fimbo ya kuchezea POOL na  mshindi  wa pili Dkt. Charles Tizeba ambaye ni Mbunge wa Buchosa alipata zawadi  ya fimbo ya kuchezea pia timu ya bunge ilipata zawadi ya ngao kwa ajili  ya kukubali kwao kushiriki mashindano hayo. 
Mashindano  hayo yalidhaminiwa na bia ya Safari Lager ilikuwa ni kati ya timu ya  bunge na combine ya TBL na TAPA yalifanyika Jumamosi iliyopita mjini  Dodoma.
Na Anna Nkinda – Maelezo, Dodoma. 
No comments:
Post a Comment