Social Icons

Sikiliza Tone Radio Live Hapa, na Tembelea Website yetu www.toneradiotz.com

bre

Tuesday, April 26, 2011

Tafakuri Yangu Ya Leo: Hawa Nao Walilelewa Na Nyerere?



……hapa hatukuja kutazamana sura kama unampenda kanywe chai….
 Pengine  watanzania wengi hawaifahamu kauli hii na hawajawahi kuisikia hata siku moja na hawajui nani aliisema? Kumbukumbu za kihistoria zinaeleza kuwa kauli hii ilielezwa naa hayati baba wa taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere katika moja ya vikao vya chama ambapo kundi Fulani lilianza kumpanda jamaa fulani ili ateuliwa sasa kuna jamaa mmoja alizidisha kusifia ikafika sehemu akaanza kumshawishi Nyerere amteue huyo rafiki yake eti kwa kuwa ana sura nzuri tena ni kijana hapo ndipo Nyerere akapandwa na hasira kisha akamwambia ..hapa hatukuja kutazamana sura kama unampenda kanywe nae chai..
   Huyu ndio Nyerere hakuwa na kawaida ya kulea tatizo , alipenda kusema ukweli pasipo kuchelewa, hakumwogopa mtu bali Mungu, ni Nyerere huyuhuyu aliwahi kuandika kitabu kilichokwenda kwa jina la Tanzania na Hatima ya Uongozi wetu  mnamo mwaka 1994 ambapo alikosoa vikali ubabaishaji katika serikali tena kwa kuwataja majina wababaishaji wote naam! Huyu ndiye Nyerere mwanaharakati aliyeishi ukweli na haki.
   Imeibuka tabia ya baadhi ya viongozi wa leo kujitapa hadharani kuwa wamelelewa na kupikwa kisiasa na kimaadili na Mwalimu Nyerere tena wengine tambo zao zinaenda mbali zaidi wanadai kuwa hata baba wa taifa aliwatabiria kuwa wao watakuwa viongozi wa kitaifa kwa maana nyingine wanataka kuwaaminisha watanzania kuwa utabiri wa Nyerere umetimia kwao.
    Lakini katika tambo zao hizi kuanzia huko kwenye CCM mpaka serikalini tunatumia vigezo rahisi tu kuwapima hawa wanaodai wamelelewa na Nyerere, hata wakijipamba vipi bado hawavutii , hata wakihubiri vipi watu hawasikilizi na hata wakijisifu vipi bado hawaheshimiki , wanatumia fedha kununua sifa lakini bado tupu watu hawawapendi , mabaya yanawafuata, hawana jema la kujivunia, inasikitisha sana.
     Wenye hekima wanapigwa na butwaa kama kweli watu hawa wamelelewa na Nyerere kama wanavyodai? Au ndio watafiti twende Butiama kwenye maktaba ya mzee huyu labda ametuachia orodha ya watu ambao mwenyewe aliwaita manyang’au hawafai kuwa viongozi hata mabalozi wa nyumba kumi? Hawa wanaohalalisha uporwaji wa ardhi huku wakiupaka rangi ya uwekezaji  wamelelewa na Nyerere yupi? Hawa waliofyatua kwa mpigo shule za kata huku watoto wao wanasoma ulaya watajifananisha vipi na Nyerere ambaye watoto wake walisoma hapahapa nyumbani? Inasikitisha kuwa Nyerere alitaka kufuta ujinga kwasababu ni adui wa taifa lakini leo hii ujinga ni mtaji wa kisiasa ndio maana tumewekewa maatabaka huku wengine wakisoma shule nzuri huko New York na Hong Kong halafu kapuku wanasota kwenye shule za kata kisha safari yao ya miaka minne inakwisha kwa kupata sifuri, inauma sana!
  Nchi inazidi kudidimia kwa rushwa , bei zinapanda kila leo, madini yanakwisha lakini wananchi hawanufaiki na maliasili zao tena siku hizi watoto wa mitaani wanaongezeka, ombaomba kibao, watu hawamudu hata milo mitatu, wapora ardhi wanaongezeka tena wanaitwa wawekezaji nasema hivi ninyi ongezeni wawekezaji ila jueni kuwa ardhi haiongezeki!
  Kisha kwa maneno mepesi walalahoi wanachagizwa kwa wimbo wa kitoto kuwa tumepiga hatua ya maendeleo, maendeleo gani? ya takwimu au ya hao viongozi kwenda kutumbuliwa vipele Berlin Ujerumani? Inauma sana! Mimi ndio maana nashangaa na nitashangaa milele watu wanaonuka rushwa kama hawa wameutoa wapi ujasiri wa kujifananisha na Nyerere? Mzee aliyeishi Ikulu kwa miaka 24 akiwatumikia watanzania kwa moyo wote aliingia masikini akatoka masikini mzee wa watu akasahau hata kujenga nyumba mpaka pale JWTZ walipoamua kumjengea, sasa amepumzika pale Butiama watanzania wanamlilia kwa ukarimu na wema wake, nathubutu kusema hao wanaojifananisha naye sidhani hata kama wanajua hata njia ya kwenda Butiama, waijue ya nini? wakafanye nini? wakati wananuka rushwa na mzee hakupenda rushwa, halafu wanaweka Nyerere Day nauliza ya nini? waache walalahoi waandae Nyerere Day yao ambapo watamkumbuka kiongozi wao wenyewe wakaendelee kuuza migodi na ardhi.
   Hawa wanagundua ndani ya chama chao kuna mafisadi lakini hawana jipya wanakuja na unafiki uliopita kiasi eti wanataka kutuaminisha kuwa nchi hii inayumbishwa na watu watatu tu? Huu ni uongo mkubwa watu watatu sio gamba peke yao wako wengi sana wote watoke na washtakiwe kwa ubadhirifu sio kuleta mzaha hapa halafu wanajifanya kumuenzi Nyerere , Nyerere hakuwa mnafiki wala mwoga alisema waziwazi. Kama kuandika tushaandika sana lakini kama ilivyo hulka ya viongozi wetu wameweka pamba masikioni hawana kawaida ya kusikiliza bilashaka kwa jinsi walivyosaliti mafundisho ya Nyerere na kumsaliti mzee huyu kwa uovu wao kuna kila dalili kuwa Nyerere anapindukapinduka kwa huzuni huko kaburini, laana yake inawaandama je tutaendelea kutawaliwa na viongozi wenye laana mpaka lini?.....Tafakari!

3 comments:

Anonymous said...

wazee wengi waliokuwa wakuu wa idara mbalimbali enzi za Nyerere wamekufa masikini bila kuwa na nyumba, na hata waliostaafu wanatia huruma, siku hizi mtu anapata kazi kwa kuwa mtoto wa mkubwa au fisadi fulani na mwaka mmoja miwili huyo mtu ni milionea, wapo wachache wanaopata kazi kihalali, kazi ipo

Anonymous said...

Ahaa wa kwetu naona umechoka kuishi au na wewe ni shushu siri ya serikali? Kuongea huko unajua unatishia maisha ya viongozi wote Tanzania, kwani ni ukweli mtupu. Ni kweli mpaka sasa unaona watoto wote wa wakubwa ndio wanalisi viti karibu vyote vya serikali, yaani majina yote ni yale yale hamna jipya bongo, bali ni mida tu imebadilika. Na kweli wanaweza kuongoza kwa sababu wamesoma abroad kutumia ushuru wa walala hoi, kwa hiyo hapo wanawazidi watoto waliosoma bongo kila kitu, hata uweke mizani gani, wako mbele. Lakini vile vile wapo WaTanzania kibao wanampinga Mwalimu kabisa kwani wanasema ujamaa wake umechelewesha maendeleo. Mimi namsuport mwalimu daima kwani aliona mbali. Utakuta watu wengi wanaompinga Mwalimu ni wasomi, na hata wakati fulani wa mchafuko wa muungano bungeni, Mwalimu mwenyewe alisema kuna wabunge wachache ndio walikuwa wanafiki. Na Tanzania, dunia nzima ya sasa imebadilika kusema kweli. Ulimwengu mzima unaelekea kwenye ubepari, yaani wachache wanatajirika kuliko wengi, na wengi ambao masikini wanakufa njaa. Tanzania na mali ya asili zote hizo tusingekuwa masikini namna hii. Uongozi umeoza.

Goodman Manyanya Phiri said...

Nimevutiwa sana kusoma kuhusu huo uwazi (CANDOUR/OPONNESS) wa Nyerere. Nafikiri Afrika kote hiyo CANDOUR ndiyo ishara (HALLMARK) ya kiongozi mzuri.